Tanzania emblem
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

JESHI LA KUJENGA TAIFA -JKT

Vijana wa Jeshi la Kujenga Taifa

Jeshi la kujenga Taifa(JKT) limekuwa linapokea na kuendesha Mafunzo yahusuyo Ulinzi wa Taifa, uzalendo, Ujasiliamali, Ujasili (kupitia mafunzo ya Kilimo, Ufugaji na Biashara) kwa nyakati tofauti tofauti kadri ya maelekezo kutoka Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Vijana wa JKT wamegawanyika katika makundi mawili nayo ni;

1. Vijana wa Kujitolea na

2. Vijana wa Mujibu wa Sheria.

Vijana wa Kujitolea: 

Hawa ni vijana wa JKT ambao wanajiunga na JKT kwa Mkataba wa kujitolea kwa kipindi kisichopungua miaka miwili (2). Mara baada ya kuandikishwa vijana hao huwa wanapelekwa kwenye kambi mbalimbali za JKT kwa ajili ya Malezi na Mafunzo mbalimbali.

Vijana wa Mujibu wa Sheria:

Hawa ni wale vijana wanaojiunga na JKT kwa mujibu wa sheria. Kwa mujibu wa katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, wanatumikia JKT kwa kipindi kisichopungua miezi (3). kwa sasa vijana wa Mujibu wa sheria ni wale wanafunzi waliomaliza kidato cha sita (form six) kutoka mashule mbalimbali ya Tanzania Bara. 

Masharti ya kijana wa kujitolea kwa ajili ya kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa.

1.Awe raia wa Tanzania

2.Awe na Umri kati ya miaka 18-23

3.Awe amemaliza darasa la saba na kuendelea

4.Asiwe ameoa au kuolewa na asiwe na mtu yeyote anayemtegemea

5.Awe tayari kufuata sheria zote za kijeshi zitazokuwa juu yake wakati akiwa jeshini(kutoroka,wizi,ulevi,uvutaji bangi, madawa ya kulevya na upatikanaji wa mimba n.k) Jeshini ni makosa makubwa na utaweza kushtakiwa na kufutiwa mkataba na JKT

6.Awe tayari kurudi nyumbani baada ya kumaliza mkataba wake na Jeshi la Kujenga Taifa

7.Awe na tabia na mwenendo mzuri

Masharti ya kijana wa mujibu wa sheria kwa ajili ya kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa.

1.Awe raia wa Tanzania

2.Awe na Umri kati ya miaka 18-35

3.Awe amemaliza kidato cha sita na kuendelea

4.Awe tayari kufuata sheria zote za kijeshi zitazokuwa juu yake wakati akiwa jeshini(Uvutaji bang, madawa ya kulevya na upatikanaji wa mimba atashitakiwa na kufutiwa mkataba na JKT

5.Utoro haukubaliki na kosa la utoro mkataba utasogezwa mbele

6.Awe na tabia na mwenendo mzuri

 

UJUE UTARATIBU WA KUJIUNGA NA JKT.

JKT huandikisha vijana wa kujitolea kutoka mikoa yote ya hapa nchini kila mwaka. Utaratibu unaotumika ni kwa JKT kuandika barua kwa wakuu wa Mikoa na kuanisha nafasi ambazo mkoa umetengewa.

Baada ya Mkoa kupata barua kutoka kwa Mkuu wa JKT na idadi ya nafasi za vijana waliopangiwa kujiunga. Mkoa hugawa nafasi hizo kulingana na wilaya zake. Pia wilaya zinatakiwa kupeleka katika tarafa, kata na vijiji. Mara nyingi uongozi wa wilaya hubandika tangazo la nafasi hizo katika ubao wao wa matangazo. JKT hutangaza nafasi za kujiunga na jeshi hilo kupitia vyombo vya habari vya Serikali na biafsi kwa nia ya kuharakisha taarifa kuwa. kia wananchi hasa vijana. Usaili wa awali hufanyika chini ya Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya wanakotoka vijana hao, baadaye hufanyika mkoani, ili kupata idadi ya vijana wa mkoa mzima.

Zoezi hilo linapokamilika mikoani, JKT hutuma timu za maafisa na askari kutoka Makao Makuu ya JKT kwa ajili ya kuhakiki vijana waliosailiwa katika mikoa yote ya Tanzania Bara. Vijana hupimwa afya zao na kusafirishwa katika vikosi vya JKT.